Wednesday, July 27, 2011

Wabunge kama Ze komedy

BUNGE la Tanzania linakoelekea
sasa si kuzuri. Pengine ndivyo
inavyoweza kuzungumzwa
kuhusu mambo yanavyokwenda
ndani ya chombo hicho cha
kutunga sheria na kuisimamia
Serikali.
Hali hiyo inatokana na tukio la
juzi usiku baada ya wabunge au
Mbunge asiyefahamika, kughushi
saini ya Waziri Mkuu, Mizengo
Pinda, wakati kikao kikiendelea.
Aliyeweka wazi aibu hiyo ni
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri
Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge,
William Lukuvi, muda mfupi
baada ya Bunge kupitisha
Makadirio ya Matumizi ya Wizara
ya Kilimo, Chakula na Ushirika
kwa Mwaka 2011/12
yaliyowasilishwa Jumatatu na
Waziri Profesa Jumanne
Maghembe, ambapo Sh. bilioni
258.3 ziliidhinishwa.
Baada ya Mwenyekiti wa Bunge,
ambaye pia ni Mbunge wa
Kibakwe, George Simbachawene
(CCM) kuzungumzia kupitishwa
kwa bajeti hiyo na kumpongeza
Waziri na wabunge, huku
akijiandaa kusitisha shughuli za
Bunge ikiwa ni karibu saa 2:15
usiku, alisimama Waziri Lukuvi na
kuomba Mwongozo wa
Mwenyekiti.
Katika maelezo yake ya kuomba
Mwongozo, Lukuvi alisema
kumeibuka tabia ndani ya Bunge
ambayo si ya kistarabu, kwani
baadhi ya wabunge wamekuwa
wakiandika ujumbe kwenye
vikaratasi kuonesha mhusika
fulani anaitwa wakati hakuna
jambo kama hilo.
“Kwa leo (juzi) hapa yametokea
matukio mawili ya wabunge
Joseph Selasini (Rombo-
Chadema) na Leticia Nyerere (Viti
Maalumu-Chadema) kupelekewa
ujumbe kwa nyakati tofauti
ukionesha umesainiwa na Waziri
Mkuu akiwaita.
“Lakini jambo la ajabu Waziri
Mkuu mwenyewe hajui lolote na
anashangaa jambo hili maana
hakuandika ujumbe kuwaita,”
alisema Waziri Lukuvi na
kusababisha mshangao kwa
baadhi ya wabunge.
Kutokana na mazingira hayo,
aliomba suala hilo liachwe na
kwamba si tabia nzuri ambayo
imeanza kujitokeza.
Akizungumzia suala hilo,
Simbachawene naye alilaani
jambo hilo na kusema kwa vile
karatasi iliyoandikwa alikuwa
nayo, itakuwa rahisi kumbaini
mhusika na kumshughulikia.
“Karatasi yenyewe imeandikwa
hivi: Mheshimiwa Joseph Selasini,
naomba uje kuna jambo tujadili,
nahitaji ufafanuzi kutoka kwako
- Mizengo Pinda,” alisema
Simbachawene na kuongeza
kuwa karatasi hiyo imesainiwa
kuonesha aliyesaini ni Waziri
Mkuu.
“Ndiyo maana nilimwona
Mheshimiwa Selasini amekwenda
kwa Waziri Mkuu akiwa
amejikunyata kistaarabu kuona
ameitiwa kitu gani, lakini
Mheshimiwa Waziri Mkuu wala
alikuwa hamfuatilii, alikuwa
ameelekeza mawazo yake katika
majibu ya Waziri,” alisema
Mwenyekiti huyo.
Alieleza kuwa jambo hilo ni la
aibu kubwa kwa wabunge,
kufikia hatua ya kughushi saini
ya Waziri Mkuu na kusisitiza
lazima ichukuliwe uzito
unaostahili.
Tangu Bunge la 10 lianze,
kumekuwa na malalamiko
kutoka kwa wadau mbalimbali
kwamba limepoteza heshima
kutokana na baadhi ya wabunge
kufanya mambo ambayo
hayaendani na chombo hicho –
ya kitoto.
Masuala ya kuzomeana, kupigana
vijembe na wakati mwingine
kuzungumza bila mpangilio, ni
baadhi ya mambo yanayopigiwa
kelele na wadau kwamba
yanakivunjia heshima chombo
hicho, ambacho ni moja ya
mihimili mikuu mitatu ya Dola.

SERIKALI IMEONGEZA TSH.2100 KATIKA MSHAHARA

SERIKALI imeongeza mshahara
wa sh 2,100 kwa watumishi
wake wa kima cha chini na sh
86,000 kwa wafanyakazi wa
ngazi ya juu.
Kwa mujibu wa taarifa
iliyotolewa kwa vyombo vya
habari jijini Dar es Salaam jana,
kima cha chini kimekuwa sh
150,000 badala ya sh 135,500
huku kima cha juu kikiwa sh
2,158,000 badala ya 1,895,740
kwa mwezi.
Kupitia taarifa hiyo Katibu Mkuu
wa Ofisi ya Rais Menejimeti ya
Utumishi wa Umma, George
Yambesi, alisema mbali na
ongezeko la asilimia 11, kuna
watumishi wengine
wameongezwa kwa wastani wa
asilimia 8.6.
Alisema mbali na kima cha chini
kuongezwa kwa sh 2100 ambao
ni ngazi ya TGTS A.1 hadi TGTS
A.8, wapo watumishi wengine
waliopata nyongeza ya sh 5,200
kutoka ngazi ya TGTS B .1 hadi
TGTS B.8.
Akitaja ngazi zingine za
mishahara kuwa ni pamoja na
ngazi ya TGTS C.1 hadi TGTS C.12
waliongezewa sh 7,000.
Aidha alisema ngazi ya TGTS D.1
hadi TGTS D.10 wameongezewa
sh 9,100, ngazi ya TGTS E.1 hadi
TGTS E .10, sh 12,000; ngazi ya
TGTS F.1 hadi TGTS F. 10 sh
20,600; ngazi ya TGTS G.1 hadi
TGTS G.12, sh 23,200; na ngazi ya
TGTS H.1 hadi TGTS H. 12, sh
42,000.
“Marekebisho haya yanawahusu
watumishi wa serikali kuu,
watumishi wa serikali za mitaa,
watumishi walioshikizwa
kwenye taasisi za umma pamoja
na watumishi ambao watakuwa
kwenye likizo inayoambatana na
kuacha kazi au kumaliza
mikataba baada ya Julai mwaka
huu,” alisema Yambesi kutipia
taarifa hiyo.
Aidha alisema watumishi
wanaopata mishahara binafsi
ambayo ni mikubwa kuliko ile ya
vyeo vyao halisi watahusika na
marekebisho haya iwapo vyeo na
mishahara yao itaangukia katika
vyeo na ngazi mpya za
mishahara.

Monday, July 25, 2011

Chadema yahaha kutatua mgogoro wa madiwani Arusha

KATIKA kile kinachoonekana ni
kutafuta suluhu ya mgogoro wa
madiwani wa Chadema katika
Halmashauri ya Jiji la Arusha,
Mwenyekiti wa chama hicho,
Freeman Mbowe amefika hapa
juzi kwa lengo la kukutana nao.
Hata hivyo, hakufanikiwa kwani
alishauriwa kutozungumzia
mgogoro huo kwa kuwa yupo
katika ngazi ya Kamati Kuu ya
chama hicho.
"Ni kweli Mbowe alikuwapo hapa
tangu Jumamosi, lengo lake
lilikuwa kukutana na madiwani
hao lakini baadaye alishauriwa
kuwa asifanye hivyo kwa kuwa
yeye ni Mwenyekiti wa Kamati
Kuu ya Chama," mmoja wa
wabunge wa Chadema Kanda ya
Kaskazini, alilieleza gazeti hili kwa
sharti la kutotajwa jina gazetini
na kuongeza:,
“Mwenyekiti yuko hapa, nadhani
atakutana na madiwani
wanaovutana na viongozi wa
kitaifa akiwamo Katibu Mkuu, Dk
Willibrod Slaa kuhusu hatua yao
ya kufikia muafaka na kukubali
baadhi ya nyadhifa ndani ya
Baraza la Madiwani la
Halmashauri ya Manispaa ya
Arusha,” alisema mtoa habari
wetu kwa sharti la kutotajwa
gazetini.
Pamoja na mambo mengine,
mwenyekiti huyo ambaye pia ni
kiongozi wa kambi rasmi ya
upinzani bungeni alitarajiwa
kusikiliza hoja za madiwani hao
na kujadiliana nao kutafuta njia
nzuri na sahihi za kuchukua
badala ya kutunishiana misuli na
vikao vya uamuzi, kama
ilivyojitokeza kwa walioamriwa
kujiuzulu nyadhifa zilizopatikana
kutokana na muafaka wa umeya
wa jiji hilo.
Kikao cha CC ya Chadema kiliagiza
madiwani waliopata nyadhifa za
unaibu meya na uenyekiti wa
kamati kujiuzulu nafasi hizo
ndani ya siku tatu kufikia Julai
21, mwaka huu. Madiwani hao
wakiongozwa na Estomih Mallah
wa Kata ya Kimandolu na John
Bayo wa Kata ya Elerai
wamegoma kutekeleza agizo hilo
na badala yake nao wakatoa
masharti ya kuombwa radhi na
Dk Slaa na Mbunge wa Arusha
Mjini, Godbless Lema kwa madai
ya kudhadhalilishwa kwa
tuhuma za kula rushwa ili kufikia
muafaka huo na CCM.
Kwa mujibu wa mbunge huyo,
wakati jitihada za Mbowe
zikigonga mwamba, mwasisi wa
Chadema, Edwin Mtei amechukua
hatua za makusudi kumaliza
mgogoro huo kwa kuzungumza
kwa nyakati tofauti na pande
zote zinazovutana. Mtei
amekutana na madiwani hao,
Lema na uongozi wa Chadema
kuzungumzia mgogoro huo
akitaka pande hizo zinazovutana
zimalize tofuati zao kwa busara.
Mtei alikutana na madiwani hao
baada ya kumwomba afanye
hivyo ili kuumaliza kwa amani
badala ya kuvutana hadharani.
Madiwani hao wa Chadema
wilayani Arusha walikutana na
Mtei nyumbani kwake Tengeru
nje kidogo ya jiji la Arusha
mwishoni mwa wiki na kuomba
ushauri juu ya mvutano huo
unaoendelea kukipasua chama
hicho.
Alipotakiwa kuzungumzia suala
hilo, Mtei hakukiri wala kukataa
kukutana na madiwani hao.
Alisisitiza kuwa Chadema
hakiwezi kumeguka kutokana na
mgogoro huo. "Sisi (Chadema)
tuna mipango na sera zenye
matumaini kwa Watanzania,
hatuwezi kumeguka kwa
mgogoro huo."
Hata hivyo, Mtei aliwataka
viongozi wa Chadema, madiwani
wake na Lema kutumia busara
na kupunguza jazba katika
kutafuta suluhu ya mgogoro huo.
.
.
.
>>Habari kutoka katika Gazeti la Mwananchi

Kikwete apunguza msafara wake

RAIS Jakaya Kikwete ameridhia
idadi ya maofisa katika ziara zake
za nje ipunguzwe ikiwa ni hatua
ya kupunguza gharama.
Waziri wa Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa,
Bernard Membe aliliambia Bunge
mwishoni mwa wiki wakati
akijibu hoja ya kambi ya upinzani
iliyoendelea kutaka safari za nje
kwa viongozi zipunguzwe.
Membe alisema katika safari ya
hivi karibuni ya Rais Kikwete
nchini Shelisheli, idadi ya maofisa
alioongozana nao ilikuwa 34 na
kwa safari ya Afrika Kusini
ilikuwa 34.
Hata hivyo, Waziri Membe alisema
wakati mwingine, wingi wa
maofisa huzingatia na aina ya
ziara na nchi anakokwenda.
Alitoa mfano kwamba, endapo
anakwenda nchi ambayo ulinzi
wake upo shakani, idadi inaweza
kuongezeka.
Alisema, zipo ziara nyingine
kama vile za kibiashara
inawezekana akalazimika
kuongozana na ujumbe wa
wafanyabiashara.
Awali, katika kuchangia hotuba
ya makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara
yaliyopitishwa, kambi hiyo ya
Upinzani kupitia kwa Waziri
Kivuli wa Wizara ya Mambo ya Nje
na Ushirikiano wa Kimataifa,
Ezekia Wenje ilisema safari za
viongozi wa juu zinatakiwa
ziendane na hali ya uchumi.
Wenje alisema katika dhana ya
kupunguza matumizi, baadhi ya
safari za nje ambazo siyo lazima
mkuu wa nchi kwenda, awaachie
viongozi wengine washiriki kwa
kuwa msafara wa Rais nje ya
nchi una gharama kubwa
ikilinganishwa na mawaziri au
maofisa wengine wa Serikali.
“Kambi ya Upinzani inaitaka
wizara ikishirikiana na ofisi ya
Rais kuweka utaratibu wa safari
za viongozi nje ya nchi, ili
kupunguza matumizi makubwa
ya Serikali na hatimaye fedha
hizo zielekezwe katika miradi
mbalimbali ya maendeleo,”
alisema Wenje.
Hata hivyo, Serikali imekuwa
ikisisitiza kwamba safari za Rais
Kikwete nje ya nchi ni zenye
manufaa na imekuwa ikitoa
mafanikio ya ziara hizo katika
nchi mbalimbali duniani.
Kwa mfano, Marekani ambako
Rais Kikwete amekuwa na ziara
tangu wakati wa utawala wa
Rais George W. Bush na sasa Rais
Barack Obama, Tanzania
imenufaika kwa kupatiwa fedha
nyingi katika miradi ya barabara,
umeme, afya na maji.

Monday, July 18, 2011

mwalimu aliyemteka mwanafunzi atishia kumuua

MWALIMU raia wa Uganda, Paul
Lubega (27) anayetuhumiwa
kumuiba mwanafunzi Ibrahim
Laurence (7) wa Shule ya Msingi
ya Mchepuo wa Kiingereza ya
Samaria ya mjini Moshi,
amesisitiza kutaka kulipwa Sh
milioni 3.5 ili amrejeshe,
vinginevyo atamuua mtoto huyo.
Kwa mujibu wa babu wa
mwanafunzi huyo, Moses
Laurence, mtuhumiwa huyo
alipiga simu tena Jumapili usiku
akisisitiza azma yake ya kulipwa
fedha hizo.
“Huyu mwalimu amempigia simu
mke wangu, Elinaike Moses
akiulizia kama fedha hizo
zimepatikana. Lakini pia alisema
hataki kuwasiliana na simu ya
zamani, bali wanunue namba
mpya kisha ndipo wamtafute,”
alisema Mzee Laurence jana
alipozungumza na gazeti hili.
Laurence alisema, mtuhumiwa
huyo ametoa muda hadi kufikia
Julai 21, mwaka huu awe
amepewa fedha hizo, vinginevyo
atakuwa amemuua mtoto huyo
na kurejesha maiti katika familia
hiyo.
“Sasa sisi tumepata wakati
mgumu, maana mama (bibi)
anatumia mtandao ambao
mtuhumiwa ndiyo anataka uwe
wa kuwasiliana naye (Airtel)
….ametoa muda hadi Alhamisi
awe amepewa hizo fedha
vinginevyo tutapokea maiti,”
alisema babu huyo.
Alisema, kutokana na taarifa hiyo,
mkewe alikwenda kutoa taarifa
Kituo cha Polisi Majengo kwa ajili
ya kuomba msaada zaidi, lakini
hadi kufikia jana mchana
hapakuwa na taarifa za
kupatikana kwa mtoto au
mtuhumiwa huyo.
Akizungumzia tukio hilo, Meneja
wa Shule ya Samaria, Batholomeo
Bigendako alisema, mtuhumiwa
huyo hakuwa mwalimu wa
kudumu shuleni hapo, bali
aliomba kazi ya kufundisha kwa
muda Kiswahili.
Tukio la kuibwa kwa mtoto huyo
lilitokea Julai 14, saa 9:30 alasiri
shuleni hapo baada ya shule hiyo
kufungwa kwa ajili ya likizo.
Inadaiwa mtuhumiwa ambaye
pia ni mwanafunzi wa Chuo
Kikuu cha Makerere nchini
Uganda akisomea taaluma ya
Ualimu, aliondoka na mtoto huyo
na haikujulikana alipokwenda.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa
Kilimanjaro, Absalom Mwakyoma,
alisema hadi sasa mtoto huyo
hajapatikana ingawa jeshi hilo
linafanya juhudi kubwa za
kumsaka.
Akielezea mazingira ya tukio,
alisema Julai 15, Laurence
alipigiwa simu namba
+254739665740 na kumuuliza
kama anamfahamu mtoto
Ibrahimu, lakini alipoulizwa kama
yupo na mtoto huyo hakujibu
tena na alikata simu na
hakupokea tena hata
alipopigiwa.
Kamanda Mwakyoma alisema,
Julai 16, saa 12 jioni, familia hiyo
ilipokea simu nyingine yenye
namba 025675361094 na mtu
anayedhaniwa ni mtuhumiwa
akitaka alipwe Sh milioni 3.5.
Kamanda huyo ameomba mtu ye
yote mwenye taarifa juu ya
mhalifu huyo atoe taarifa kupitia
namba 0754 293349, 0787
550996 au atume ujumbe
kupitia namba 0767 750175 na
atazawadiwa.

Sunday, July 17, 2011

viongozi 6 wa dini wakiri kujihusisha na dawa za kulevya

VIONGOZI sita wa madhehebu ya
dini wanaojihusisha na biashara
haramu ya dawa za kulevya
nchini, wamejitokeza mbele ya
Kamati ya Maadili ya Viongozi wa
Dini na Haki za Jamii na kukiri
kujihusisha na biashara hiyo kwa
muda mrefu sasa.
Kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la
Polisi, baada ya kuhojiwa,
viongozi hao waliiomba Kamati
hiyo kutowataja hadharani
majina ama madhehebu yao kwa
kuhofia kubezwa kwa
madhehebu wanayoyaongoza.
Akizungumza mwishoni mwa
ziara yao Zanzibar, Mwenyekiti
wa Kamati hiyo, Mchungaji
William Mwamalanga wa Kanisa
la Pentekoste Tanzania, alisema
mbali ya orodha hiyo, ipo pia ya
watu 18 wakiwemo
wafanyabiashara wakubwa na
wanasiasa wanaojihusisha na
biashara hiyo.
Alisema orodha zote zitafikishwa
kwa Mkuu wa Kitengo cha Polisi
cha Kupambana na Dawa za
Kulevya nchini.
Mchungaji Mwamalanga alisema
tatizo la ongezeko la dawa za
kulevya, pia inazihusu nchi
mbalimbali duniani na kwamba
kamati hiyo itakutana na kamati
nyingine kama hizo za nchi za
Maziwa Makuu kuzungumzia
ufumbuzi wa suala hilo.
Alisema mkutano huo pia
utapendekeza kwa mabunge ya
nchi hizo na Bunge la Afrika
Mashariki kutunga sheria za
kuwafilisi wote waliojilimbikizia
mali kutokana na biashara za
dawa za kulevya kwa nchi
wanachama.
Hata hivyo, Kamati hiyo ya Maadili
ya Viongozi wa Dini na Haki za
Jamii ikiwa Visiwani, imesifu na
kupongeza juhudi za Jeshi la
Polisi kwa hatua zao za
kukabiliana na ongezeko la dawa
za kulevya.
Akizungumzia kero ya dawa za
kulevya visiwani hapa, Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Mjini
Magharibi, Aziz Juma Mohammed,
alisema Jeshi hilo limekuwa
likiwakamata wengi wa
wafanyabiashara na watumiaji
wa dawa za kulevya na
kuwafikisha mahakamani.
Hata hivyo, Kamanda Aziz alitoa
mwito kwa wananchi na wadau
mbalimbali wa usalama
kuendelea kusaidiana na Jeshi
hilo kwa kutoa taarifa za wale
wote wanaojihusisha na
mtandao wa dawa hizo.
Kamanda Aziz alisema kama kila
mwananchi atatoa taarifa za siri
Polisi za kuwepo kwa mtu ama
kundi la watu wanaojihusisha na
biashara hiyo ama uhalifu
mwingine wowote, ni wazi kuwa
Polisi itawatia mbaroni.
Wiki iliyopita, watu wawili
wakazi wa Dar es Salaam,
wamekamatwa kwenye Uwanja
wa Ndege wa Kimataifa wa
Abeid Amaan Karume, Zanzibar
kwa nyakati tofauti wakitokea
Brazil, ambapo kila mmoja
alipatikana na kiasi kikubwa cha
dawa za kulevya aina ya kokeini.

Wednesday, July 13, 2011

MAREKANI YAONYA RAIA WAKE KWENDA SUDAN KUSINI

Marekani inawaonya raia wake
hatari ya kusafiri kuelekea Sudan
Kusini licha ya maadhimisho ya
uhuru katika nchi hiyo mpya.
Ubalozi wa Marekani nchini
Sudan kusini uliwasihi
wamarekani Jumanne kutosafiri
kuelekea mikoa ya mpakani kati
ya Sudan na Sudan kusini
ikielezea mapigano ya karibuni
kati ya majeshi yanayotii wakuu
wa nchi hizo mbili pamoja na
kuongezeka kwa majeshi pande
zote za mpaka.
Ubalozi unasema ukiongezea
mapigano hayo ya ardhini, jeshi
la anga la Sudan limepiga
maeneo ya mpaka katika
majimbo ya Unity na Kordofan
kusini. Ubalozi pia umeonya
hatari ya ghasia katika maeneo
yote ya Sudan kusini ikisema
kuna majeshi tofauti ya waasi
yasiyopungua saba ambayo mara
kwa mara yanapambana na
majeshi ya Sudan kusini.
Ubalozi unasema serikali ya
Sudan kusini ina uwezo kiasi wa
kupambama na uhalifu nje ya mji
mkuu wa Juba na kwamba hata
hapo walipo hatari ya ghasia za
uhalifu zipo juu.
Sudan kusini imekuwa taifa jipya
siku ya Jumamosi baada ya
wakazi wake walipopiga kura
kwa wingi kujitenga kutoka
kaskazini katika kura ya maoni ya
mwezi Januari.
Sudan ilipigana vita vya wenyewe
kwa wenyewe kwa miaka 21
ambavyo vilimalizika mwaka
2005. Sudan na Sudan kusini
bado wana mizozo kadhaa
ambayo haijatatuliwa ikiwemo
nani atadhibiti mkoa wa Abyei
wenye utajiri wa mafuta na
namna ya kushirikiana katika
mapato ya mafuta.

SITA;''wapinzani ni wanafiki''

WAZIRI wa Ushirikiano wa Afrika
Mashariki, Samuel Sitta, amesema
mambo mengi ya wapinzani ni
ya kinafiki na wamekuwa
wakiibeza Serikali kwa kauli
nyepesi nyepesi.
Sitta alitoa kauli hiyo jana
bungeni mjini Dodoma
alipokuwa akijaribu kutuliza
Bunge lililokuwa limechafuka
baada ya Mbunge wa Kigoma
Kusini, David Kafulila (NCCR-
Mageuzi), kudai kuwa Serikali
iliyoko madarakani ni legelege na
imeshindwa kukusanya kodi.
"Nawasihi wenzangu hasa wa
CCM, hawa wapinzani hii
(kupinga mambo) ndiyo kazi yao,
wanabeza kila tunachofanya kwa
lugha nyepesi nyepesi na mambo
mengi wanayozungumza ni
unafikinafiki hivi, sisi tuwaachie
wananchi wawahukumu.
Kauli hiyo ilisababisha baadhi ya
wabunge hasa wa upande wa
upinzani kusimama na kuomba
mwongozo wa Mwenyekiti na
wengine wakizomeana, huku
Sitta ambaye ni Kaimu Kiongozi
wa Shughuli za Serikali Bungeni,
akiwa amesimama akiomba
kuendelea.
"Subirini nitoe mfano ...
wanazungumza posho za vikaoni
ni kuibia wananchi na baadhi
yao wamekuwa wabunge kwa
miaka mitano iliyopita na
walikuwa wakizichukua, kama
kweli ndivyo hivyo, basi
warudishe," alisema Sitta.
Kauli hiyo ilisababisha wabunge
zaidi, karibu 10 wakiwamo wa
CCM kusimama kuomba
Mwongozo wa Mwenyekiti, lakini
Mwenyekiti Jenista Mhagama
akaahirisha shughuli za Bunge
kwa mapumziko ya mchana, kwa
kuwa muda ulikuwa umefika,
huku akiwaacha wabunge
wakipiga kelele za kuomba
Mwongozo.
Kabla ya kuibuka tafrani hiyo,
Kafulila aliyekuwa akichangia
hotuba ya Makadirio ya Matumizi
ya Wizara ya Afya na Ustawi wa
Jamii, alisema tangu Uhuru moja
ya maadui waliopigwa vita ni
maradhi; lakini akashangaa
bajeti ya Afya ni ndogo na
kuongeza kuwa inatokana na
Serikali legelege kushindwa
kukusanya mapato.
"Miaka 50 ya Uhuru asilimia 90
ya bajeti ya maendeleo ya afya
inategemea fedha za nje, tatizo
hamkusanyi kodi na Nyerere
(Baba wa Taifa) alisema Serikali
legelege inashindwa kukusanya
kodi," alisema Kafulila.
Kauli hiyo ilipingwa na Mbunge
wa Nzega, Dk. Hamisi Kigwangala
(CCM) aliyesema Kafulila alitumia
neno la kuudhi kwa kuiita
Serikali ya CCM legelege.
Dk. Kigwangala alifafanua kuwa
Kafulila hakuwa na taarifa sahihi,
kwa kuwa katika miaka mitatu
iliyopita, Serikali ilikuwa
ikikusanya karibu Sh bilioni 200,
lakini mpaka mwaka huu,
makusanyo yaliongezeka na
kufikia karibu Sh bilioni 400.
Baada ya ufafanuzi huo,
Mwenyekiti wa Bunge, Mhagama
alimtaka Kafulila kufuta usemi,
lakini mbunge huyo alipinga
akisema ni kauli ya Baba wa
Taifa, ambaye kila mtu
anamuenzi bila kujali anatoka
chama gani.
"Tunapoteza muda kujadili suala
ambalo liko wazi, mwaka
2005/06 Serikali ilikuwa
ikikusanya wastani wa Sh bilioni
260 lakini dola moja ilikuwa
sawa na Sh 1,000.
"Leo mnakusanya karibu Sh
bilioni 400 kwa mwezi, dola
moja ni Sh 1,600 ni hesabu
rahisi, hakuna kilichoongezeka ...
sifuti usemi, niko tayari kufia
ukweli huu," alisema Kafulila na
kusababisha Sitta kuamka na
kuwaita wapinzani wanafiki
huku akiwataka CCM
kuwavumilia.
Hata hivyo, Mwalimu Nyerere
alisema chama legelege huzaa
Serikali legelege na pia aliwahi
kusema "Serikali corrupt
(inayokula rushwa) hushindwa
kukusanya kodi," na si Serikali
legelege hushindwa kukusanya
kodi.
Awali, kabla ya tafrani hiyo,
Kafulila alimtaka Waziri wa Afya
na Ustawi wa Jamii, Dk. Hadji
Mponda, ikibidi ajiuzulu kuliko
kukubali kuwasilisha bajeti ya
fedha ndogo bungeni huku
ikitegemea fedha nyingi za
wahisani.
Alisema hiyo inatokana na
wabunge na familia zao kuwa na
uwezo wa kutibiwa sehemu
yoyote ndani na nje ya nchi,
ndiyo maana hawawekezi katika
hospitali za vijijini.
Wakati akisema hayo, mmoja wa
wabunge ambaye hakufahamika
lakini mwanamke, aliwasha
kipaza sauti akasema: "Pamoja
na wewe (Kafulila) na Mbunge
wa Mpanda Mjini Chadema (Said
Arfi ambaye alilazwa India hivi
karibuni)."
Hata hivyo Waziri wa Nchi Ofisi ya
Waziri Mkuu, Uwekezaji na
Uwezeshaji, Dk. Mary Nagu,
alisimama na kupinga kauli ya
Kafulila, akisema: "Hili ni Bunge
Tukufu, tuzungumze kwa
heshima."
Mbunge mwingine mwanamume
akawasha kipaza sauti na kuhoji:
"Nani ana heshima?" Nagu
akaendelea kufafanua kuwa
mwanawe ni daktari katika
Hospitali ya Taifa ya Muhimbili
ambayo ni ya Serikali na hata
baba yake mzazi alilazwa katika
hospitali ya Katesh ambayo ni ya
vijijini.
Hata hivyo, sauti ile ya kiume
iliendelea kumkatisha Nagu na
safari hii Mbunge huyo alisema,
"so what(kwa hiyo?"
Kutokana na kauli hizo za
kukatishana, Mhagama alisimama
na kusema ameisikiliza sauti ya
mmoja wa wabunge wanaotoa
kauli hizo za kejeli huku
akimkatisha waziri aliyekuwa
akizungumza na kubaini kuwa
sauti hiyo inafanana na ya
Mbunge wa Nyamagana, Ezekia
Wenje (Chadema).
Alionya kuwa wanachofanya
wabunge kuwasha vipaza sauti
holela ili kuzuia hoja za wenzao
kusikika au kuwakatiza, ni
kinyume na Kanuni za Bunge na
akifuatilia anaweza kuwabaini na
kuwachukulia hatua.

Tuesday, July 12, 2011

TANESCO YAELEZA KILICHOSABABISHA UMEME KUKATIKA UWANJA WA TAIFA

SHIRIKA la Umeme Tanzania
(Tanesco), limesema hitilafu za
kiufundi zilisababisha kutokea
kwa hitilafu ya umeme juzi katika
sehemu kubwa nchini na
kusababisha mikoa kadhaa kuwa
gizani kwa takriban saa tano.
Aidha, Tanesco imesema kituo
cha kupokea, kupoza na
kusambaza umeme cha Ilala, Dar
es Salaam kilipata hitilafu na
hatimaye kusababisha
kukosekana kwa umeme kwenye
Uwanja wa Taifa, wakati wa
fainali ya Kombe la Kagame kati
ya Yanga na Simba.
Meneja Uhusiano wa Tanesco,
Badra Masoud alisema hayo jana
katika taarifa yake kwa vyombo
vya habari na kueleza kuwa
hitilafu hiyo ilianza kujitokeza saa
12:53 jioni baada ya kituo cha
kupokea, kupoza na kusambaza
umeme cha Ilala kupata hitilafu.
Alisema, kutokana na hitilafu hiyo
maeneo ya Kurasini, Kigamboni,
Mbagala, Mkuranga na Uwanja
wa Taifa yalikosa umeme.
Alisema, mafundi wa shirika hilo
walitatua tatizo hilo ambapo
waliwaunganisha wateja wa
Uwanja wa Taifa kutokea katika
kituo kingine kilichopo Kurasini,
na umeme ulirejea uwanjani saa
1:20 usiku.
Hata hivyo, alisema baadaye
umeme ulikatika tena kutokana
na kukatika kwa Gridi ya Taifa
kutokana na sababu za kiufundi
zilizosababishwa na kukatika
kwa kiunganishi cha laini
iliyokuwa ikitokea katika kituo
cha kuzalisha umeme cha New
Pangani na kusababisha gridi
yote kuzimika hadi kupelekea
mikoa yote iliyoungwa nayo
kukosa umeme.
Alisema, kutokana na hitilafu
hiyo, mafundi walitengeneza na
kurejesha umeme katika hali
yake ya kawaida saa 6:30 usiku
na tatizo hilo kwa sasa
limekwisha kutatuliwa na
maeneo yote yana umeme
isipokuwa wale ambao wapo
katika mgawo ambao ratiba yake
ilishatangazwa.
“Uongozi wa shirika unaomba
radhi kwa hitilafu hiyo ya umeme
iliyotokea jana (juzi) ambapo
maeneo mengi yalikosa umeme
hususan kuleta usumbufu
mkubwa kwa mashabiki wa
mpira na wadau wengine,”
alisema Badra katika taarifa hiyo
ya Tanesco.

Friday, July 1, 2011

PINDA AMJIBU LOWASA

WAZIRI Mkuu Mizengo Pinda
ameliambia Bunge kuwa serikali
ya Awamu ya Nne haiogopi
kufanya maamuzi na
imeshafanya maamuzi mengi
magumu.
Alikuwa akijibu hoja za wabunge
waliochangia hotuba ya bajeti ya
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda,
akiwamo aliyekuwa Waziri Mkuu,
Edward Lowassa ambaye
aliituhumu Serikali kwa
kushindwa kufanya maamuzi
magumu.
Akizungumza kwa mara ya
kwanza bungeni tangu
alipojiuzulu wadhifa huo kwa
kashfa ya Richmond Februari 7
mwaka 2008, Lowassa
aliishangaa Serikali kwa kuogopa
kufanya maamuzi.
Lowassa aliyeshika Uwaziri Mkuu
Desemba 30, mwaka 2005 akiwa
Waziri Mkuu wa Kumi nchini,
akiichambua zaidi Serikali
bungeni hivi karibuni alisema
viongozi wa Serikali wameingiwa
na ugonjwa wa kuogopa kutoa
maamuzi kwa mambo
mbalimbali hatua inayokwamisha
utekelezaji wa miradi ya
maendeleo.
Lakini katika majibu yake ya jana
jioni, Pinda alisema Serikali haina
cha kuogopa na kwamba tayari
imeshafanya maamuzi mengi
tena mengine ni magumu.
Alisema moja ya maamuzi hayo
ni uamuzi wa kuvunja Baraza la
Mawaziri uliotokana na yeye
Lowassa kujiuzulu.
“Halikuwa jambo jepesi hata
kidogo bali ni moja ya maamuzi
mazito ambayo yamefanywa na
Serikali ya Awamu ya Nne.
Inataka Moyo…” alisema Pinda.
Pinda alisema maamuzi hayo ni
sehemu ya maisha ya Serikali
katika kutekeleza majukumu
yake kwa dhana ya Uwajibikaji
wa pamoja, yaani Collective
Responsibility kupitia Baraza la
Mawaziri.
“Tunachohitaji ni kuvumiliana.
Kuvuta subira, kwani mambo
mema hayataki haraka!
Tutaamua na tutafanya,” alisema
Pinda na kuongeza; “Napenda
kulifahamisha Bunge lako Tukufu
kwamba Serikali ya Awamu ya
Nne chini ya Mheshimiwa Rais
Dk. Jakaya Mrisho Kikwete ndiyo
pekee imefanya maamuzi
magumu na mazito kuliko zote
zilizopita.”
Aliyataja maamuzi mengine kuwa
ni pamoja kuimarisha Utawala
Bora, akitolea mfano uamuzi
mgumu wa kuwafikisha
mahakamani waliokuwa
mawaziri wa Serikali zilizopita
kutokana na tuhuma mbalimbali
zinazowakabili za kutumia
madaraka isivyo halali.
Baadhi ya mawaziri wa Awamu
ya Tatu waliofikishwa
mahakamani kutokana za
matumizi mabaya ya madaraka ni
pamoja na Basil Mramba
aliyekuwa Waziri wa Fedha na
Daniel Yona (Nishati na Madini)
na aliyekuwa Katibu Mkuu wa
Wizara ya Fedha, Gray Mgonja.
Pinda aliendelea kusema
kwamba, Serikali ya Awamu ya
Nne ndiyo iliyoamua kujenga
shule za sekondari za Kata
ambazo zimewezesha wanafunzi
wengi kupata elimu ya
sekondari.
“Leo tumeshuhudia kuwa kati ya
wanafunzi 20 tuliowapongeza
kwa kufanya vizuri kwenye
mitihani ya kidato cha sita 2011,
saba (7) wanatoka shule za Kata,
sawa na asilimia 35,” alisema.
Aliongeza kuwa, wameweka
historia ya kuamua kujenga Chuo
Kikuu cha Dodoma ambacho ni
kikubwa mno nchini na kwamba
faida yake inaonekana, kwani
tayari zaidi ya wanafunzi 20,000
wanasoma kwa sasa.
“Ninaamini kila mmoja kati yetu
humu ndani anaye mtoto, awe
mjukuu, mjomba, shangazi, baba
mdogo, ndugu, jamaa na hata
rafiki tu ambaye anasoma katika
chuo hiki.
Ndiyo sababu kubwa
inayotufanya wote tuone
uchungu wa baadhi ya watu
wanaowasumbua hivyo
kusababisha watoto wetu
washindwe kukamilisha masomo
yao kwa wakati kutokana na
migomo inayojitokeza mara kwa
mara.
“Aidha, tunajenga Chuo cha
Serikali za Mitaa Hombolo
ambacho kimefikia hatua nzuri,”
alisema Pinda na kuongeza kuwa
Serikali ya Awamu ya Nne
imekamilisha miradi yote 27 ya
barabara kuu zilizoanzishwa na
Serikali ya Awamu ya Tatu.
Sasa hivi unaweza kutoka
Mtwara-Dar es Salaam-Dodoma
hadi Mwanza kwa kupitia
kwenye barabara ya lami.
Alisema pia kwamba, Serikali
imeamua fedha zote za MCC
zipelekwe kujenga barabara za
mikoa iliyoko pembezoni.
“Tumeshuhudia ndani ya Bunge
hili waheshimiwa wabunge, bila
ya kujali itikadi za vyama
wakisifu maendeleo
yaliyopatikana kule Kigoma.
Maamuzi mengine ni Ujenzi na
ukamilishaji wa miradi ya maji
cchini. Tumefanya maamuzi
mazito katika kuwalinda watu
wenye ulemavu wa ngozi na
tumefanikiwa,” alisema.
Waziri Mkuu alisema ili kuondoa
mpasuko wa kisiasa Zanzibar,
“tumefanya maamuzi magumu
ya kukubali kuanzisha Serikali ya
Umoja wa Kitaifa katika Serikali
ya Mapinduzi Zanzibar.


KWA HABARI KAMILI SOMA GAZETI LA HABARI LEO LA KESHO

Thursday, June 30, 2011

MADIWANI JINO KWA JINO NA DK SLAA

MADIWANI wa Chadema katika
Manispaa ya Arusha, wamesema
chama hicho ‘hakina ubavu’ wa
kuwafukuza kwa kuwa kufanya
hivyo, kitakuwa kinacheza
mchezo wa pata potea.
Wakizungumza na Gazeti la Habari leo la nchini Tanzania kwa
masharti ya kutotajwa majina
gazetini baada ya kuonywa
kutozungumzia mgogoro wao
na uongozi wa chama hicho
Taifa, madiwani hao walisema
wanaamini Kamati Kuu ya chama
hicho haiwezi kufanya kosa hilo.
‘’Hili suala linapaswa kuamuliwa
kwa hekima na busara,
kunifukuza mimi ama madiwani
wote hapa kuna mambo mawili;
moja Chadema kupoteza viti
vyote ama kupata na hiyo ni
bahati nasibu na sidhani kama
Kamati Kuu italikubali hilo,’’
alisema mmoja wa madiwani
hao.
Juni 29 Katibu Mkuu wa
Chadema, Dk. Willibrod Slaa,
alikaririwa akisema chama hicho
kiko tayari kuwatimua madiwani
wake wote wa Arusha kwa
madai kuwa wamekisaliti chama
baada ya kufikia muafaka wa
Arusha kwa maslahi ya mkoa
huo.
Dk. Slaa alikaririwa, akisema
uamuzi wa madiwani huo,
kumpata meya na naibu wake
Arusha ambao ulipongezwa na
Baraza la Vijana la Chadema
(Bavicha), hawautambui kwa
madai una upungufu ukiwamo
wa kukosa barua ya Chadema ya
kukubali maridhiano.
Baada ya kauli hiyo ya Dk. Slaa,
iliyotolewa baada ya kauli
nyingine ya Mbunge wa Arusha,
Godbless Lema, kwamba
hatambui maridhiano hayo ya
amani na yenye lengo la
kuharakisha maendeleo ya
Arusha, madiwani hao Juni 30
waliweka kikao katika hoteli
moja
kubwa mjini hapa kujadili kauli
hizo.
Baada ya kikao hicho, diwani
mwingine alisema Dk. Slaa
amewatumia ujumbe kwa njia ya
mtandao wa intaneti na
kuwaamuru waache
kuzungumzia suala hilo katika
vyombo vya habari.
Alisema hata hivyo, kikao chao
kimesisitiza kuwa muafaka
waliofikia na madiwani wenzao
wa CCM, ni sahihi uliofuata
taratibu zote kwa maslahi ya
chama na si uamuzi wa mtu
binafsi wenye uroho wa
madaraka na kamwe
hawakukurupuka.
‘’Tumefikia muafaka kwa maslahi
ya Chadema pia, hatukufanya
hivyo kwa uroho wa kutaka vyeo
katika kamati ndani ya
Halmashauri.
Kauli kwamba tuliamua kwa
uroho wa madaraka ni kutaka
kuupotosha umma na kauli hizo
hazifai kutamkwa na kiongozi
kama Lema,’’ alisema diwani
huyo.
Alisema wanawaheshimu sana
viongozi wao wa juu, lakini na
wao ni viongozi waliochaguliwa
na wananchi kama Lema na
uamuzi waliochukua Lema
anaujua, lakini inasikitisha kuona
madiwani wakiamua ni kosa,
wakati ni kwa maslahi ya wakazi
wa Arusha.
Diwani huyo alidai Lema anajua
kila kitu, kwa kuwa katika
mchakato wa awali,
alishirikishwa na kuambiwa kila
kitu kinachoendelea, lakini
hakutoa uamuzi ila
kinachoonekana ni ubinafsi
wake na huo ndio unaosumbua
ndani ya Chadema.
‘’Hapa suala ni kutoa uamuzi kwa
maslahi ya chama na si mtu
binafsi; hilo halitawezekana,
kwani kila mmoja anapaswa
kuheshimiwa na kusikilizwa
katika kutoa uamuzi na
wasitokee baadhi ya watu ndani
ya chama kuonekana miungu
watu,’’ alisema.
Mbali na Dk. Slaa na Lema, pia
Mwenyekiti wa Chadema,
Freeman Mbowe, alinukuliwa
kwa nyakati tofauti akipinga
muafaka huo.
KWA HABARI ZA UHAKIKA ZAIDI SOMA GAZETI LA HABARI LEO!

Sunday, June 26, 2011

AZALILISHWA KWA KUDUNGWA SINDANO SEHEMU YA HAJA KUBWA

JESHI la Polisi mkoani Rukwa
linamtafuta mwanamke mmoja
mkazi wa mtaa wa Lwiche
Kitongoji cha Mazwi katika
Manispaa ya Sumbawanga kwa
tuhuma ya kumchoma sindano
iliyowekwa maji ya moto mtoto
mwenye umri wa miaka sita
kwenye sehemu yake ya haja
kubwa kwa madai kuwa ni
kikojozi.
Mwanamke huyo aitwaye Severia
Mpepo anatuhumiwa kumfanyia
unyama huo mtoto huyo na
kumsababishia maumivu makali
juzi majira ya saa moja asubuhi.
Kitendo hicho kisicho kawaida
kilisababisha mtoto huyo ambaye
ni wa kiume kupiga kelele za
kuomba msaada kutoka kwa
majirani kabla ya kuzimia na
kukimbizwa na wasamaria katika
Hospitali ya Mkoa wa Rukwa kwa
ajili ya matibabu.
Kwa mujibu wa majirani wa
mtoto huyo ambao hawakutaka
kutajwa majina yao walisema
kuwa tukio la kuunguzwa
linafuatia mateso mfululizo
aliyokuwa akiyapata kutoka kwa
mama mlezi wake, Severia
ambaye amekuwa akimlea kwa
kipindi cha miezi sita tangu
kufariki kwa mama mzazi wa
mtoto huyo.
Majirani hao walisema mtoto
huyo aliletwa kwa mlezi huyo na
babake mzazi anayefahamika
kwa jina la Peter Matalanganya
kufuatia ushauri wa rafiki yake
ambaye ndiye mume wa Severia
aliyemshauri kuwa ampeleke
kwake ili apate kumlea baada ya
mkewe kufariki dunia.
“Tunasikia kuwa huyu mtoto
aliletwa hapa na babake miezi
sita iliyopita baada ya mamake
kufariki, lakini kuanzia alipofika
huyu mwanamke amekuwa
akimtesa sana mara amnyime
chakula, mara amchape na juzi
ndio kahitimisha kwa kumfanyia
huu unyama wa kumwunguza
katika sehemu yake ya haja
kubwa, kwa kweli huyu mama
hafai na ni muuaji mkubwa,“
walisema majirani hao.
Kwa upande wake Mganga Mkuu
wa Mkoa wa Rukwa, Dk. Saduni
Kabuma alikiri kumpokea mtoto
huyo hospitalini hapo na
kupatiwa tiba ambapo katika
uchunguzi alionekana kuwa
ameunguzwa katika sehemu za
haja kubwa na maji hayo kiasi
cha kumsababishia
malengelenge.
Dk. Kabuma alisema kuwa taarifa
alizopata kutoka kwa ndugu wa
karibu waliomfikisha hospitalini
hapo zimedai mama mlezi wa
mtoto huyo alichukua uamuzi
huo wa kinyama kwa kuwa
kijana ni kikojozi wa kupindukia.
Naye Daktari aliyempokea mtoto
na kumpatia huduma ya
matibabu katika kitengo
wagonjwa wa nje, Dk. Revocatus
Kasoni alisema kuwa hali ya
mtoto huyo inaendelea vizuri na
kuongeza kuwa bado yupo
katika uchunguzi wa kitabibu
zaidi.
Alipoulizwa na waandishi wa
habari waliofika nyumbani
kwake kutaka kufahamu undani
wa tukio hilo alikiri kutenda
unyama huo, lakini alisema
hakutenda kwa makusudi bali
alikuwa anampatia mtoto huyo
tiba ya ugonjwa wa tumbo kwa
kumpiga bomba.
Kamanda wa Polisi mkoani
Rukwa Isuto Mantage
alipoulizwa kuhusu tukio hilo
alisema kuwa mama huyo bado
hajakamatwa na Jeshi hilo
linaendelea kumsaka mama huyo
ili sheria ichukue mkono wake
iwapo ikibainika kuwa alitenda
uovu huo.
....

Thursday, June 23, 2011

TATIZO LA MISHAHARA KWA WALIMU KUISHA MWAKANI

KUANZIA mwaka ujao wa fedha,
walimu wa shule za msingi na
sekondari hawatapata tena
matatizo ya kupata mishahara
mara wanaporipoti kazini.
Katibu Mkuu wa Tamisemi,
Hussein Kattanga amesema,
mwaka huu yametokea matatizo
ambayo yalisababisha baadhi ya
walimu kushindwa kulipwa
mapema mishahara yao ndio
maana yakatokea matatizo hayo.
“Tumejipanga kuhakikisha kuwa
mwalimu anaporipoti katika
kituo chake cha kazi analipwa
stahili zake zote,” amesema
Kattanga.
Amesema, wakurugenzi
watendaji watapelekewa fedha
hizo haraka na kwenye mfumo
wao wa malipo utakuwa
umeunganishwa moja kwa moja
Wizara ya Utumishi pamoja na
Fedha.
Alikuwa akizungumza kuhusu
maadhimisho ya Siku ya Serikali
za Mitaa mwaka 2011 ambayo
kitaifa yatafanyika mkoani
Rukwa Julai mosi mwaka huu na
mgeni rasmi atakuwa Waziri
Mkuu Mizengo Pinda.
Alisema, maadhimisho hayo
yatazinduliwa leo na Mkuu wa
Mkoa wa Rukwa, Daniel ole
Njoolay mjini Sumbawanga.
Alifafanua kuwa lengo la Serikali
kugatua madaraka na kuziweka
shule hizo kwenye ngazi ya
halmashauri ni kutaka kutatua
matatizo kama hayo ya walimu
kwa haraka.
Alisema, licha ya sherehe ya
kitaifa kufanyika Sumbawanga,
lakini kila halmashauri itafanya
sherehe hizo katika eneo lao ili
kutoa fursa ya wananchi wa
maeneo husika kwenda kutoa
kero zao.
Alitoa mwito kwa wananchi
kujitokeza kwa wingi katika
maeneo ambako sherehe hizo
zitafanyika ili waelimishwe haki
zao na majukumu ya Serikali za
Mitaa.
Kaulimbiu ya maadhimisho ya
mwaka huu ni mafanikio ya
Serikali za Mitaa katika miaka 50
ya Uhuru yatumike kuimarisha
ugatuaji wa madaraka kwa
wananchi kwa maendeleo yao.
Alisema, Serikali iliamua kutenga
siku maalumu kuadhimisha
sherehe hizo kila mwaka ili
kuwahabarisha wananchi juu ya
umuhimu wa serikali za mitaa,
nafasi na wajibu wao kwa
serikali za mitaa, pia kuwahimiza
wananchi kuhusu utekelezaji wa
shughuli za maendeleo kwa
lengo la kuchochea ukuaji wa
uchumi na kupunguza umasikini.
Alisema Siku ya Serikali za Mitaa
inatoa fursa kwa kila
halmashauri kuonesha shughuli
mbalimbali zinazotekelezwa
katika mamlaka zao.

MKULIMA ATUHUMIWA KUMBAKA MWANAFUNZI

POLISI mkoani Singida
wamemkamata mkulima, Iddi
Ramadhan (20) mkazi wa kijiji
cha Matyuku Singida Vijijini, kwa
tuhuma za kumbaka mwanafunzi
wa shule ya sekondari na
kumsababishia maumivu makali.
Kamanda wa Polisi mkoani
humo, Celina Kaluba, amesema,
Ramadhan alikamatwa Juni 18
mwaka huu saa moja jioni katika
kitongoji cha Makyunje, Kata ya
Mtamaa tarafa ya Unyakumi
Manispaa ya Singida.
Amesema, mtuhumiwa anadaiwa
kumkamata kwa nguvu binti
huyo mwenye miaka 15, kumziba
mdomo na kumkokota hadi
kichakani na akamvua nguo yake
ya ndani na kumfanyia unyama
huo.
Kamanda Kaluba amesema, mara
baada ya kukamilika kwa
upelelezi, mtuhumiwa
atafikishwa mahakamani kujibu
tuhuma inayomkabili.
Katika tukio lingine, Kaluba
amesema, Polisi wamemkamata
mkulima mkazi wa Mang'onyi,
Singida Vijijini, Saidi Msengi (22)
kwa tuhuma ya kumgonga kwa
pikipiki mwendesha baiskeli,
Polino Michael na kusababisha
kifo chake.
Alieleza kuwa siku ya tukio,
mtuhumiwa alikuwa akiendesha
pikipiki aina ya Sanlag T.708 BRP
na alimgonga mwendesha
baiskeli huyo Michael (50)
mkulima na mkazi wa kijiji cha
Matare.
Alisema, Polino alifariki dunia
akiwa njiani kwenda hospitali ya
mkoa kupatiwa matibabu.

KUNA UBAYA KATIKA FACEBOOK??

La hasha! Ni matunda ya kukua
kwa utandawazi. Mtanzania asiye
na pasport, leo anaweza akawa
na rafiki Australia ambaye
anakuwa anamjua kila
kinachoendelea katika Jiji la
Sydney. Hakuna gharama kubwa,
anajua yote kwa mtindo wa
kuchati kwenye ukurasa wa
Facebook.
Mtanzania akiwa nje ya nje,
akitaka kujua muhtasari wa kile
kinachoendela nchini kwake,
anaweza kutumia gharama
nafuu, kuulizia mazingira na
usalama wa taifa kupitia ukurasa
wa Facebook. Inapeleka watu
katika ulimwengu mpya,
inazidisha uhalali wa usemi
kwamba dunia ya sasa ni kama
kijiji kimoja.
Inasaidia kuongeza wigo wa
marafiki. Watu wanaweza
kubadilishana mawazo ya kijamii,
pia wakapeana uzoefu kwa
namna mbalimbali.
Inawakutanisha watu kwa njia
ya kipekee na kuwafanya
wazoeane kabla ya kugeuka
marafiki wakubwa.
INA ATHARI GANI KIMAPENZI?
Facebook imekuwa ikiwafanya
baadhi ya wanaume kuona njia
ya mkato kupata wapenzi wa
mbali. Akaunti yake inajaza
marafiki wa kike, hana mpango
na wanaume wenzake.
Wanakuza wigo wa kunufaika
katika ngono.
Msomaji na rafiki yangu, Shadya
Ismail aliniandikia ujumbe kwa
SMS ambao unasomeka hivi:
“Simu ni tatizo lakini huku
kwenye Facebook nako ni balaa.
Kusema ukweli, mimi nikigundua
mpenzi wangu anatumia muda
mwingi internet lazima
nimfuatilia nijue kinamsumbua
nini.”
Nilipomuuliza kwanini, alijibu:
“Hakuna amani Facebook.
Mwanaume anaomba urafiki kwa
mwanamke na anamkubalia.
Wakikutana online wanachati,
wanakubaliana baadhi ya vitu na
ikiwezekana wanapanga mpaka
miadi ya kukutana. Amini
kwamba hayo yapo na kuna
watu ni mfano.”
Nikamuomba ufafanuzi:
“Mapenzi ya siku hizi
hayatabiriki, nadhani ndiyo
maana tunaambiwa hizi ni
nyakati za mwisho. Watu
hawajuani lakini wanazoeana
kwa kuchati kisha wanakuwa
wapenzi. Nasema kwa kujiamini
kwa sababu nimetongozwa na
wengi.”
Anasimulia alivyotongozwa:
“Kuna wanaume watatu
waliniomba urafiki kwenye
Facebook. Mimi nikikuta ombi
nakubali. Siku tukikutana online,
tunachati vizuri lakini maswali
mengi yanakuwa yale binafsi
zaidi, yaani kama vile mtu
anataka kukujua sana.
“Nashindwa kutilia hofu,
kwahiyo najibu. Mwisho wa yote
anamalizia kwa kukutaka
kimapenzi. Watu watatu
wamenitongoza na kusitisha
urafiki nao. Ninao marafiki
wawili wa kike, mmoja amewahi
kulala kimapenzi na jamaa
aliyekutana naye Facebook,
alipopata penzi alianza mbele.
“Mwingine mpaka leo
anaendelea na mpenzi wake
ambaye walikutana Facebook.
Lakini huyo mpenzi wake ni
mume wa mtu, kwahiyo
wanaibana. Hapo utaona ni kwa
namna gani fursa za watu
kukaribiana kimapenzi
zimeongezeka hasa baada ya
Facebook kuchanua.”
SHADYA ANASEMA KWELI
Ni ukweli kwamba Facebook
inaumiza watu kwenye mapenzi.
Idadi ya watu wanaoanzisha
uhusiano mpya ni kubwa kila
siku kupitia kurasa hizo.
Uaminifu umekuwa ukipungua
na wasiwasi wa watu kwa
wapenzi wao ni kubwa.
Ninao mfano wa jamaa mmoja
ambaye kila anapofungua
ukurasa wa mwenzi wake, yeye
hukimbilia kuangalia marafiki
wapya ambao amewasajili.
Huumizwa mno anapogundua
kuna midume imo kwenye
orodha. Wanagombezana lakini
ushahidi wa kusaliti haupo.
Mwingine yeye hufuatilia namna
mwenzi wake anavyojadiliana na
marafiki zake katika mada
mbalimbali. Akiona picha ya
mpenzi wake imesifiwa mno na
mwanaume, anahoji:“Huyu
mbona amekusifia sana, ni nani
wako? Lazima mtakuwa
mnajuana, haiwezekani iwe hivi
hivi.”
SULUHISHO
Kila mmoja anatakiwa aishi kwa
maumivu ya mwenzi wake. Ni
vizuri pia akawa na uelewa
mpana kwamba hakuna kitu
kibaya kama kumfanya
mwenzako kuwa na wasiwasi na
wewe. Fanya kila uwezalo lakini
hakikisha mpenzi wako
anakuamini muda wote.
Atakuamini kama humpi sababu
ya kukutuhumu. Haoni tatizo
Facebook, rafiki mwenye
maneno yasiyofaa, jaribu
kumpotezea mapema.
Anapofungua ukurasa wako,
hakuti kitu kibaya zaidi ya
marafiki ambao mazungumzo ni
ya kawaida.
Kwanini ulegee kwa kuchati peke
yake? Onesha msimamo. Kama
wewe ni bachela si vibaya
ukianzisha uhusiano lakini ikiwa
una mwenzi wako, epuka.
Kumbuka kwamba jinsi ilivyo
kwako kupata mpenzi, naye
hivyo hivyo ni rahisi kunasa
wake. Unaona hatari iliyopo?
Uaminifu siyo tu kwamba ni kitu
muhimu, bali pia ni nguzo ya
uhusiano wowote ule. Ukiwa
chanzo wewe ukateleza,
utaachwa au ukisalitiwa
itakuuma na hata uamuzi
utakaouchukua, hautaweza
kufidia maumivu uliyoyapata.

BEI YA MAFUTA YA TAA KUPANDA MARA 7

MAFUTA ya taa na maji ya
kunywa ya chupa yatapanda bei
kutokana na uamuzi wa Serikali
kupandisha ushuru wa bidhaa
hizo.
Kupanda kwa mafuta ya taa ni
dhahiri kutawasononesha
Watanzania wengi hasa vijijini,
lakini Serikali imejitetea kuwa
uamuzi huo umechukuliwa ili
kuepukana na uchakachuaji
mafuta, ambao umeelezwa kuwa
unaididimiza nchi kiuchumi.
Akiwasilisha Muswada wa Sheria
ya Fedha mwaka 2011, Naibu
Waziri wa Fedha, Pereira Silima,
alisema jana kuwa Serikali
imeongeza ushuru wa bidhaa
kwa mafuta ya taa kutoka Sh 52
hadi Sh 400.30.
Uamuzi huo unaondoa tofauti
iliyokuwapo kati ya bei ya dizeli
na bei ya mafuta ya taa na pia
utadhibiti uchakachuaji wa dizeli
ambao hufanywa na
wafanyabiashara kwa
kuchanganya dizeli na mafuta ya
taa, ili kujipatia faida kubwa, kwa
kuwa kodi au bei kwenye mafuta
ya taa ni ndogo.
Eneo hilo la kupandisha bei ya
mafuta ya taa lilipokewa kwa
hisia tofauti na wabunge
ambapo Mbunge wa Bariadi
Magharibi, Andrew Chenge (CCM)
alipongeza hatua hiyo kwa
maelezo kuwa bei ndogo ya
mafuta hayo ilikuwa inanufaisha
watu wachache hasa
wafanyabiashara.
Lakini Mbunge wa Mbozi
Mashariki, Godfrey Zambi (CCM),
alitaka Serikali isipandishe
ushuru wa mafuta ya taa, kwani
ndiyo yanategemewa na
wananchi wengi vijijini.
Amesema, kisingizio cha
kupandisha ushuru huo kwa
kuogopa wachakachuaji,
kinaonesha dhahiri kuwa Serikali
imeshindwa kuwadhibiti
wachakachuaji hao.
Kwa upande wa maji ya kunywa
ya chupa, kinywaji hicho
kimewekwa kwenye kundi la
vinywaji baridi ambavyo ushuru
wake utapanda kutoka Sh. 63,
hadi Sh. 69 kwa lita. Uamuzi huo
utapandisha bei ya maji ya
kunywa ya chupa kama ilivyo
kwa soda na juisi.
Eneo hilo lilipata upinzani kutoka
kwa wabunge, akiwamo
Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha
na Uchumi, Dk. Abdallah Kigoda,
ambaye wakati akiwasilisha
maoni ya Kamati hiyo, alisema
maji ya kunywa ya chupa
yasiongezwe ushuru.
“Tunaishauri Serikali kutoongeza
ushuru kwa bidhaa hizo, kwani
yanatumika na wananchi wengi
wa vijijini na mijini … ni bidhaa
muhimu na ya lazima,” alisema
Kigoda.
Dk. Kigoda amesema, bidhaa hiyo
ya maji imesaidia kupunguza
maambukizi yaliyokuwa
yakisababishwa na maji yasiyo
salama katika baadhi ya maeneo
nchini.
Chenge katika eneo hilo, alisema
maji ya chupa kutokana na
kuuzwa bei ya chini wananchi
wengi wa vijijini wanayatumia
na kupunguza magonjwa ya
kuhara, hivyo yasiongezwe
ushuru.
Katika Muswada huo wa fedha,
Serikali pia imepunguza kwa
kiwango cha asilimia 50 tozo za
mamlaka mbalimbali, ikiwamo
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma
za Maji na Nishati (EWURA),
Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri
wa Nchi kavu na Majini (Sumatra)
na Shirika la Viwango (TBS)
kwenye bidhaa za mafuta.
Amesema, kwa upande wa tozo
za aina hiyo zinazotozwa na
taasisi zingine kama Shirika la
Kusafisha Mafuta (Tiper),
Mamlaka ya Mapato (TRA) na
Mamlaka ya Bandari (TPA), Silima
alisema mikataba na hati husika
zitafanyiwa marekebisho ili
kutekeleza hatua hiyo ya Serikali
ya kupunguzo tozo hiyo kwa
asilimia 50.
Pia alisema ushuru wa mafuta ya
petroli kwa sasa na tozo zote
zitalipwa kwa kutumia sarafu ya
Tanzania au fedha za kigeni
zinazoweza kubadilishwa katika
shilingi ya kitanzania, ambayo
kwa mujibu wa utaratibu wa
Benki Kuu ya Tanzania (BoT),
malipo hayo yanaruhusiwa kwa
dola ya Marekani pekee.
Kuhusu kiwango cha faini ya
makosa ya usalama barabarani,
Serikali imepunguza kiwango
hicho kutoka Sh. 50,000 ya awali
hadi Sh. 30,000.
Amesema lengo la hatua hiyo ni
kuongeza adhabu kwa
watakaovunja sheria za
barabarani, ili kupunguza
ongezeko la ajali.
Hata hivyo, kiwango hicho
kiliendelea kupingwa na
wabunge na kambi ya Upinzani
ikitaka kiwango cha awali cha Sh.
20,000 kiendelee kwani Sh.
30,000 ni kubwa. Nayo Kamati ya
Fedha na Uchumi ilipinga kiasi
hicho na kutaka kishuke hadi Sh.
25,000.

NAPE AMPONGEZA MBOWE KURUDISHA SHANGINGI

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa
Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya
CCM, Nape Nnauye,
amempongeza Kiongozi wa
Kambi ya Upinzani bungeni,
Freeman Mbowe, kwa kusikia
mwito wa chama hicho na
kuamua kurudisha gari la Serikali
alilokuwa akilitumia.
Nape ambaye yupo katika ziara
ya kutembelea vyombo vya
habari nchini, amemtaka Mbowe
kuendelea kutekeleza mwito wa
CCM wa kuhakikisha wafanyakazi
wa Chadema, akiwamo Katibu
Mkuu wa chama hicho, Dk.
Willibrod Slaa, wanalipa kodi
inayotokana na kipato chao
(PAYE).
Nape alitoa kauli hiyo jana
alipokuwa akijibu swali baada ya
kuzungumza na uongozi wa
Kampuni ya Tanzania Standard
Newspapers Ltd (TSN),
inayochapisha magazeti ya Daily
News, Sunday News, HABARI LEO
na HABARILEO Jumapili.
“Anaona aibu kutembelea gari
lililonunuliwa na walipa kodi
wakati Chadema hailipi kodi,
ndiyo maana karudisha kwa
kukosa uhalali wa kulitumia, ni
vema atekeleze mwito wa kulipa
kodi na akimaliza, tutamwambia
mengine ili wajisafishe,” alisema
Nape.
Alikumbusha kuwa CCM ndiyo
iliyoanzisha hoja ya Mbowe
kurudisha gari la Serikali
analotumia. "Mtakumbuka
Chadema walikwenda
Sumbawanga na kuwaambia
wananchi kuwa Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda, anatembelea gari
la kifahari.
“Lakini nilipokwenda kule
(Sumbawanga), nilifafanua kwa
wananchi kuwa Mbowe baada ya
kupata cheo cha Kiongozi wa
Upinzani Bungeni, alichukua gari
la gharama kubwa mara tatu ya
gari la Waziri Mkuu,” alisema
Nape.
Kutokana na gharama za gari
hilo la Mbowe, Nape alikumbusha
kwamba alimtaka Mbowe
alirudishe serikalini, ili apewe
gari la gharama ndogo na
kumshukuru kwa kutekeleza
mwito huo juzi alipotangaza
kulirudisha.
Alifafanua, kwamba amekuwa
akiwataka Chadema kuishi kwa
kauli zao na kuepuka kusema
mambo ambayo wao wenyewe
hawayaamini wala
hawayatekelezi.
“Wanapiga kelele watu walipe
kodi, lakini TRA (Mamlaka ya
Kodi), imesema Chadema
haijawahi kulipa kodi tangu
imeanzishwa,” alisema Nape.
Akieleza zaidi tabia hiyo ya
Chadema, ya kusema
wasichotenda, Nape alisema
Mbowe pia aliagiza magari
yaliyotumika na kuyatumia
wakati wa kampeni na baada ya
uchaguzi.
Kwa mujibu wa Nape, Mbowe
alilazimisha Chadema itumie
ruzuku, ambayo ni fedha ya
Serikali, kununua magari hayo
aliyoyatumia huku akijua wazi
kuwa kuna sheria inayokataza
Serikali kununua vitu
vilivyotumika.
Nape pia aliutaka uongozi wa
TSN kuendelea kuandika ukweli
na kuepuka habari zilizotiwa
chumvi na pia iibue maovu hata
ndani ya Serikali, ili kuisaidia
kutekeleza Ilani ya CCM.
Akijibu hoja ya Kaimu Mhariri
Mtendaji wa TSN, Mkumbwa Ally,
kuhusu kampuni hiyo kuidai
Serikali madeni makubwa, Nape
alisema atalifikisha hilo katika
vikao vya chama ili Serikali
itekeleze wajibu wake kwa
kulipa matangazo iliyoyatoa.

Tuesday, June 14, 2011

MKULO;SINA UWEZO WA KUONDOA POSHO

Wakati wanaharakati wakipinga,
Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo,
amesema hana uwezo wa
kuondoa posho za Mbunge wa
Kigoma Kaskazini (Chadema),
Zitto Kabwe, na wenzake wa
NCCR- Mageuzi wanaotaka
ziondolewe.
Akizungumza mjini
Dodoma jana, Mkulo alisema
Baraza la Mawaziri pekee ndilo
lenye uwezo wa kutengua sheria
hiyo na si yeye hivyo
wanaomtaka azihamishe
hawajui wanachosema.
" Mimi Mkulo sina uwezo wa
kubadilisha maamuzi ya baraza la
mawaziri hata siku moja, suala
likishaamriwa kule mtu binafsi
huna uwezo wa kulitengua,
labda niende kwenye baraza hilo
nijenge hoja wakubali,” alisema.
Katika hatua nyingine, Mkulo
alishangaa hatua ya wabunge
wanaokataa posho hizo
zipelekwe kwenye majimbo yao
badala ya kuiachia serikali
uamuzi.
" Kama wanataka zifutwe
waseme, lakini kusema ziende
sehemu fulani haina maana,
kama kweli wanataka kubana
matumizi waseme posho hizi
zifutwe na wafuate taratibu
maana ziko kwa mujibu wa
sheria za nchi,”alisisitiza Mkulo.
" Zitto ni mjumbe wa kamati ya
uongozi ya Bunge kama kweli
hataki hizi posho angesema kule
zikatwe sasa mbona alishiriki
kuzipitisha? "alihoji.
Wabunge wa Chadema na
wengine wanne wa NCCR-
Mageuzi wote kutoka majimbo
ya Mkoa wa Kigoma, wanataka
posho hizo zifutwe.
Akizungumzia posho hizo za
vikao, Mbunge wa Vunjo (TLP),
Agustine Mrema, alisema kwa
kuwa serikali ilishatangaza katika
bajeti yake kuwa itapunguza
posho zisizo za lazima, basi
itaangalia kama posho za
wabunge nazo hazina ulazima.
" Mimi naunga mkono posho
zisizo za lazima ziondolewe,
kama serikali itaona posho za
wabunge si za lazima na
ikaziondoa mimi sina neno,
wakiona mbunge anaweza kuja
hapa Dodoma na akafanya kazi
zake bila kuhitaji hiyo posho
sawa mimi nasubiri uamuzi wa
serikali,” alisema.
Mbunge wa Wawi (CUF), Hamad
Rashid, alisema kuwa: " Katiba
inatamka wazi kwamba mtu
akifanya shughuli hii malipo yake
ni haya sasa tatizo ni nini."
Alisema kama wanaopokea
posho hizo wanaona hawana
haja nazo waandike hundi na
kuzirejesha zilikotoka badala ya
kupiga kelele kwenye vyombo
vya habari.
" Hizo ni cheap politics (siasa
uchara) ambazo mimi binafsi
sizitaki na kamwe sitazishabikia,
mbona wanapokwenda kwenye
halmashauri kule wanasaini
posho iweje wakija huku ndipo
waseme hawazitaki, maoni
yangu ni kwamba tukiamua
kubadili sheria na kuziondoa
sawa sitakuwa na tatizo, lakini
kwa kuwa sasa hivi ziko kisheria
tatizo linatokea wapi,” alisema
Rashid.
Spika wa Bunge, Anne Makinda,
alisema kuna watu wanapotosha
kuwa mshahara wa mbunge ni
zaidi ya milioni saba wakati
mshahara halisi ni Sh. milioni 2.5
na wanakatwa Sh. 900,000 kila
mwezi kwa ajili ya mikopo ya
magari waliyochukua.
KWA HABARI ZAIDI SOMA GAZETI LA NIPASHE LA LEO TAREH 13 JUNE