Thursday, June 23, 2011

NAPE AMPONGEZA MBOWE KURUDISHA SHANGINGI

KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa
Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya
CCM, Nape Nnauye,
amempongeza Kiongozi wa
Kambi ya Upinzani bungeni,
Freeman Mbowe, kwa kusikia
mwito wa chama hicho na
kuamua kurudisha gari la Serikali
alilokuwa akilitumia.
Nape ambaye yupo katika ziara
ya kutembelea vyombo vya
habari nchini, amemtaka Mbowe
kuendelea kutekeleza mwito wa
CCM wa kuhakikisha wafanyakazi
wa Chadema, akiwamo Katibu
Mkuu wa chama hicho, Dk.
Willibrod Slaa, wanalipa kodi
inayotokana na kipato chao
(PAYE).
Nape alitoa kauli hiyo jana
alipokuwa akijibu swali baada ya
kuzungumza na uongozi wa
Kampuni ya Tanzania Standard
Newspapers Ltd (TSN),
inayochapisha magazeti ya Daily
News, Sunday News, HABARI LEO
na HABARILEO Jumapili.
“Anaona aibu kutembelea gari
lililonunuliwa na walipa kodi
wakati Chadema hailipi kodi,
ndiyo maana karudisha kwa
kukosa uhalali wa kulitumia, ni
vema atekeleze mwito wa kulipa
kodi na akimaliza, tutamwambia
mengine ili wajisafishe,” alisema
Nape.
Alikumbusha kuwa CCM ndiyo
iliyoanzisha hoja ya Mbowe
kurudisha gari la Serikali
analotumia. "Mtakumbuka
Chadema walikwenda
Sumbawanga na kuwaambia
wananchi kuwa Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda, anatembelea gari
la kifahari.
“Lakini nilipokwenda kule
(Sumbawanga), nilifafanua kwa
wananchi kuwa Mbowe baada ya
kupata cheo cha Kiongozi wa
Upinzani Bungeni, alichukua gari
la gharama kubwa mara tatu ya
gari la Waziri Mkuu,” alisema
Nape.
Kutokana na gharama za gari
hilo la Mbowe, Nape alikumbusha
kwamba alimtaka Mbowe
alirudishe serikalini, ili apewe
gari la gharama ndogo na
kumshukuru kwa kutekeleza
mwito huo juzi alipotangaza
kulirudisha.
Alifafanua, kwamba amekuwa
akiwataka Chadema kuishi kwa
kauli zao na kuepuka kusema
mambo ambayo wao wenyewe
hawayaamini wala
hawayatekelezi.
“Wanapiga kelele watu walipe
kodi, lakini TRA (Mamlaka ya
Kodi), imesema Chadema
haijawahi kulipa kodi tangu
imeanzishwa,” alisema Nape.
Akieleza zaidi tabia hiyo ya
Chadema, ya kusema
wasichotenda, Nape alisema
Mbowe pia aliagiza magari
yaliyotumika na kuyatumia
wakati wa kampeni na baada ya
uchaguzi.
Kwa mujibu wa Nape, Mbowe
alilazimisha Chadema itumie
ruzuku, ambayo ni fedha ya
Serikali, kununua magari hayo
aliyoyatumia huku akijua wazi
kuwa kuna sheria inayokataza
Serikali kununua vitu
vilivyotumika.
Nape pia aliutaka uongozi wa
TSN kuendelea kuandika ukweli
na kuepuka habari zilizotiwa
chumvi na pia iibue maovu hata
ndani ya Serikali, ili kuisaidia
kutekeleza Ilani ya CCM.
Akijibu hoja ya Kaimu Mhariri
Mtendaji wa TSN, Mkumbwa Ally,
kuhusu kampuni hiyo kuidai
Serikali madeni makubwa, Nape
alisema atalifikisha hilo katika
vikao vya chama ili Serikali
itekeleze wajibu wake kwa
kulipa matangazo iliyoyatoa.

No comments:

Post a Comment